WHO IS WHO

Hii ni page maalum kwa wazalendo wa wilaya zetu yaani Karagwe na Kyerwa.Madhumuni ya page hii ni kutambua nani ni nani ili tuweze kufamihana na kusaidiana katika kujenga wilaya,mkoa na taifa letu na vilevile wengine walikuwa  ni wazalendo ambao wameishatangulia mbele ya haki si vibaya tukiwafahamu na kuwakumbuka.Katika page yetu unaweza kututumia picha yako na maelezo binafsi (CV)ya wewe ni nani,ukowapi,unafanya nini na ulisoma nini au unasoma nini.Tuma kupitia karagweyetu@gmail.com.

Jaji James Kateka



Alizaliwa katika Kijiji cha Nyakahanga, Wilaya ya Karagwe April 29 mwaka 1945. Nilisoma darasa la kwanza hadi la nne kwenye Shule ya Msingi ya Nyakahanga kuanzia 1952-1955. Nilifuzu na kwenda kusoma Mugeza Middle School, Bukoba darasa la tano hadi la nane kati ya mwaka 1956 na 1959.
Nilichaguliwa kujiunga na Shule ya Sekondari ya Tabora ambayo ilikuwa shule yenye hadhi kubwa na ambayo imetoa viongozi wengi. Nilisoma Tabora kidato cha kwanza hadi cha sita toka mwaka 1960 hadi 1965. Nikahitimu na kuchaguliwa kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam mwezi Julai 1966.
Oktoba 1966, tulifukuzwa Chuo kikuu cha Dar es Salaam,
kwa kufanya maandamano ya kupinga masharti tuliyowekewa kuhusu kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa. Hivyo nilipoteza mwaka mmoja. Nikahitimu na shahada na LLB (Hons) Machi 1970. Darasa letu ndilo lilifunga Chuo Kikuu cha Afrika ya Mashariki. Nilisoma na baadhi ya viongozi wa sasa kwenye nchi za Afrika ya Mashariki.
Mwaka huo wa 1970 nilijiunga na Wizara ya Mambo ya Nje mshauri wa masuala ya kisheria kwenye Idara ya Itifaki na Mikataba na wakati huo idara hiyo ilikuwa ikiongozwa na Balozi Daniel Mfinanga ambaye sasa ni marehemu.
Katibu Mkuu wa Wizara alikuwa Balozi Obed Mbogo Katikaza ambaye naye pia ni marehemu. Balozi Katikaza alikuwa ni mchapakazi hodari na aliheshimiwa sana na wafanyakazi. Mwaka 1971, ilianzishwa Idara ya Sheria kwenye Wizara na Mkurugenzi wake wa kwanza alikuwa ni Jaji Joseph Sinde Warioba ambaye nilifanya kazi naye hadi alipochaguliwa kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Pia nilikuwa naye wakati akiongoza ujumbe wa Tanzania katika vikao vya Mkutano wa Sheria ya Bahari kutoka mwaka 1971 hadi mwaka 1982.
Kati ya mwaka 1973 na 1974 nilikwenda kusomea shahada ya pili (LLM) katika sheria ya kimataifa huko King’s College, Chuo Kikuu cha London. Kati ya mwaka 1976 na 1980 nilifanya kazi kwenye ofisi yetu ya kudumu ya Umoja wa Mataifa. Balozi wangu alikuwa ni Dk. Salim Ahmed Salim ambaye nilifanya kazi naye wakati Tanzania ikiwa mjumbe wa Baraza la Usalama (Security Council) mwaka 1975 hadi 1976. Pia alichaguliwa kuwa Rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwaka 1979.
Niliporudi nyumbani, nilikuwa mkuu wa sehemu ya mikataba, kabla ya kuteuliwa kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Sheria kwa miaka sita toka mwaka 1983 hadi 1989.
Mwaka 1989 hadi 1994 niliteuliwa kuwa Balozi wa Tanzania Ujerumani. Pia niliiwakilisha Tanzania huko Austria, Uswiss Romania, Vatican na Poland. Mwaka 1994 nilihamishiwa Moscow, Urusi nilikokaa hadi 1998 nilipohamishiwa Stockholm, Sweden. Huko niliiwakilisha nchini yangu katika nchi za Denmark, Norway, Finland, Iceland na Baltic Republics (Estonia, Latvia na Lithuania). Nilikaa kwenye nchi za Nordic kwa miaka saba hadi nilipostaafu mwaka 2005.
Kwa bahati nzuri, mwaka huo wa 2005 nilichaguliwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Sheria ya Bahari (iliyoko Ujerumani), wadhifa nilioushikiria hadi sasa.
 

No comments:

Post a Comment